KUFIKIA MATARAJIO YAKO.

 

KUFIKIA MATARAJIO YAKO.



Tupo katika mchakato wa kuyaendea mafanikio yako na matarajio yako. Tukiangalia safari ya wana wa Israel inatupa maswali mengi ya kujiuliza kwa maana Biblia inasema safari yao ni kivuli cha safari yetu katika wokovu, ukitaka kujua safari yako ikoje na inaishiaje angalia safari ya wana wa Israel, itakupa mwangaza wa safari unayoiendea.

Ninapo itazama safari ya wana wa Israel nina maswali, je! Ni wangapi watakao faulu kufika mwisho wa safari yao? Wana wa Israel walikuwa wanaenda katika nchi ya dhahabu, maziwa na asali, hawakuwa na safari ya kwenda mbinguni bali ni safari ya kuendea matarajio na mbaraka wao. Kama kuna wakati wa kujiuliza maswali ni kupitia safari ya wana wa Israel ambayo kwetu sisi ndio kioo na ramani yetu ya kuelekea uzima wa milele.

Kabla haujaanza safari yako ya kuelekea katika Baraka zako ziko changamoto nyingi utakutana nazo kama vile wana wa Israel walivyokutana nazo walivyokuwa njiani, hayo yaliyowasibu na wewe ukubali au usikubali utakutana nayo kabla haujakutana na mbaraka wako, sasa swali langu ni kuwa ni wangapi watakao faulu. Je ni wangapi wataondoka katika tabia za dhambi au tabia za zamani? Biblia inasema hamjafanya vita na dhambi hata mkamwaga damu, kumbe kuna vita kati yako na dhambi na sio na shetani, huu ndio mpambano wako mkubwa na wala sio shetani au majini. Mpambano wa mtu aliyeokoka ni kati yake na dhambi huo ndio mpambano wake mkubwa ambao unabebwa na tabia za kale, tabia za mababu na tabia za watu wote na sio kwenye hayo mengine unayoyaona. Hii siyo vita ya leo bali ni vita ambayo ilianzishwa na Mungu mwenyewe baada ya anguko la Adamu na Hawa. Mwanzo 4:7 “ Kama ukitenda vyema, hutapata kibali? Usipotenda vyema dhambi iko, inakuotea mlangoni, nayo inakutamani wewe, walakini yapasa uishinde.” Hapa hakuna ibilisi wala mchawi, safari ya maisha ya mtu anayetamani kuwa na maisha yaliyo bora ana mpambano kati yake na dhambi. Dhambi inakukaribia kwa sababu ya tabia zako, sio kwa sababu ya ibilisi, wachawi wala matambiko, la! Bali ni kwa sababu ya tabia, hapo ndipo palipokuwa na mpambano wa wewe ni nani, mpambano wa kesho yako ndio uko hapo.

Adui mkubwa wa wokovu wako ni dhambi, na huyo adui ana rafiki yake mpendwa ambaye wewe ndio umemuumba, ni nani huyo? Ni tabia. Mwanzo 4:7 “ Kama ukitenda vyema, hutapata kibali? Usipotenda vyema dhambi iko, inakuotea mlangoni, nayo inakutamani wewe, walakini yapasa uishinde.” Mungu anakutamani ili moyo wako umkaribishe, lakini dhambi haihitaji uikaribishe bali tabia yako tu, kuna tabia ukiwa nayo dhambi inakukaribia na kufurahi na wewe. Biblia inasema yapaswa uishinde. Kama kuna mtihani ambao mwanadamu amepewa ni kubadilisha tabia, mabadiliko hayo ya tabia kwa mwanadamu hayajalishi ni maskini au tajiri, upo kanisani, barabarani, umeoa au umeolewa, au hujaoa au kuolewa ni mtoto au kijana, tabia haina umri wala imani. Unaweza ukawa una imani lakini tabia yako inakusababisha uwe uliyeshindwa. Unaweza ukawa hauna imani lakini tabia yako ikawa inamvutia Mungu na kusababusha akushindie. Kaini sio kwamba alikuwa hana imani, la! alikuwa nayo na ndiyo maana alikwenda kumtolea Mungu dhabihu; Mfalme Sauli alikuwa na Imani lakini kwa nini aliishia hapo alipo ishia? Shida sio imani bali ni tabia yake. Tabia yako inaweza kukupelekea kushinda au kushindwa. Jiulize nafsini mwako tabia gani unayo wewe, je! Inamvutia Mungu au mapepo na majini?.

Mungu alimpenda sana Musa, Musa alikuwa ni mtu mwenye imani na pia alikuwa anaumba imani kwa wengine, lakini aliambiwa na Mungu achukue wana wa Israel kwenda Kaanani lakini yeye mwenyewe hakuingia. Kwa nini Musa hakuingia Kaanani? Kutokana na tabia yake. Je! wewe unatabia ya aina gani? Musa alifanya dhambi gani mpaka akanyimwa kuingia Kaanani? Musa alikuwa na hasira na kwa sababu ya hiyo ikampelekea kutokufanya kama alivyoelekezwa na Mungu, alifanya hivyo mara moja tu na ikamgharimu. Ni mara ngapi wewe haukufanya kama ulivyoelekezwa na Mungu ukafanya unavyojua wewe kwa sababu ya hasira, kiburi au kujua?. Mungu akusaidie. Maombi ni akiba na yanasimama badala ya neno mbele za Mungu, yaweke maombi yako yawe kama akiba, watu wengi wanaweka pesa kama akiba lakini wewe weka maombi yako kwa Mungu kama akiba, kuna siku utakuwa hauwezi hata kuomba lakini yale maombi yako uliyoomba miaka miwili au mitatu iliyopita yatamkumbusha Bwana. Tabia ni tendo, iwe ni kwa kuwaza au kutenda. Musa pamoja na machungu yote aliyopitia kwa sababu ya wana wa Israel lakini hakuonja yale maziwa wala asali, kwa sababu gani? Kwa sababu ya tabia yake.

Mwanzo 21:9 “Sara akamwona yule mwana wa Hajiri Mmisri, ambaye alimzalia Ibrahimu, anafanya dhihaka.” Hapa nini kilitokea? Tabia iliinuka, tabia ilileta vurugu nyumbani kwa Ibrahimu. Tabia sio kwa mtoto tu, unaweza ukawa ni mtoto au mtu mzima lakini tabia itakuonyesha jinsi ulivyo. Mwanzo 21:10-12 “Kwa hiyo akamwambia Ibrahimu, Mfukuze mjakazi huyu na mwanawe, maana mwana wa mjakazi hatarithi pamoja na mwanangu, Isaka. Na neno hilo lilikuwa baya sana machoni pa Ibrahimu, kwa ajili ya mwanawe. Mungu akamwambia Ibrahimu, Neno hili lisiwe baya machoni pako, kwa ajili ya huyo mwana, na huyo mjakazi wako. Kila akuambialo Sara, sikiza sauti yake, kwa maana katika Isaka uzao wako utaitwa.” Usimdharau mkeo kwa sababu hajazaa, wala usimdharau kwa sababu yoyote ile, unakuta mtu ameoa mke baada ya muda anaanza kumuona huyo mke ana sura mbaya na hamtaki tena, usimuache mke wako kwa sababu yoyote ile; kwa sababu wakati unamuoa walikuwepo wadada wengine wazuri zaidi ya mkeo lakini wewe ukamchagua huyo. Usije ukawaona wadada wengine ni wazuri kuliko mkeo ukaona kuwa mkeo hafai hapana. Kuna wengi wameshindwa kufanikiwa kwa sababu ya tabia zao, Je! wewe mwanaume upo tayari kumsikiliza mke wako? Au wewe mwana mke uko tayari kumsikiliza mume wako? Wengi wenu Mungu hawabariki kwa sababu tu ya kutokuelewana kwenu, Mungu akiona mnagombana kila mara na hamsikilizani kamwe hatawabariki kwa sababu anaona mtauana. Ukiona ndoa inachanua jua kuwa kuna kusikilizana ndio maana Mungu anawabariki.

Mwanzo 21:14-16 “Ibrahimu akaamka asubuhi na mapema akatwaa mkate na kiriba cha maji, akampa Ha jiri akimtwika begani pake, na kijana, akamruhusu; naye akatoka, akapotea katika jangwa la Beer-sheba. Yale maji yakaisha katika kiriba, akamlaza kijana chini ya kijiti kimoja. Akaenda akakaa akimkabili, mbali naye kadiri ya mtupo wa mshale; maana alisema, Nisimwone kijana akifa; naye akakaa akimkabili, akapaza sauti yake, akalia.” Wengi mmefukuzwa mbali na Baraka zenu kwa sababu ya tabia zenu.

Tabia yako inaweza kukuzuia usizione baraka zako zilipo. Kumbu kumbu 28:3 “Utabarikiwa mjini, utabarikiwa na mashambani.” Hapo ulipo baraka zako zipo lakini je! Tabia yako inakuruhusu uzione hizo baraka? Je! tabia yako inamruhusu Mungu akubariki?.

Mwanzo 21:17 “Mungu akasikia sauti ya kijana. Malaika wa Mungu akamwita Hajiri kutoka mbinguni, akamwambia, Una nini, Hajiri? Usiogope, maana Mungu amesikia sauti ya kijana huko aliko.” Ni maombi yangu kwa Mungu kuwa akafungue macho yako ili uweze kuona zile baraka ambazo ziko karibu na wewe, kuna baraka na muujiza wako upo hapo hapo ulipo lakini ili uweze kuona lazima Mungu afungue macho yako, akisha fungua macho yako na ukaona shida yako imeisha.

Kwa nini watu wanafanya biashara alafu zinakufa? Ni kwa sababu sio kile ambacho Mungu amewapa, unakuta mtu ndani ya moyo wake tangu mwanzo ana msukumo wa kufanya biashara fulani lakini akianza kufanya hiyo biashara akiona haiendi vizuri ndipo anaanza kuwaza sijui niuze nguo au mchele, yaani anauza kila kitu; kile ambacho umesikia kutoka ndani ya moyo wako ukikifanya hicho umetoboza. Unaanza biashara si kwa sababu una hela, la! Bali unaanza kwa sababu Mungu amekupa.

Biashara yoyote ambayo Mungu amekupa hauanzi na kuwa na hela bali unaanza na wazo ndipo pesa zinakuja. Unapaswa kujiuliza maswali yafuatayo:-

  1. Je! Tabia yangu inaniruhusu mimi kuona?
  2. Je! Tabia yangu ina chelewesha Mungu kunipa yale yaliyo ya kwangu?

KUMILIKI NA KUTAWALA.



Zaburi 16:5-6 “BWANA ndiye fungu la posho langu, Na la kikombe changu; Wewe unaishika kura yangu. Kamba zangu zimeniangukia mahali pema, Naam, nimepata urithi mzuri.”

Yeyote aliye weka kura yake katika uwepo wa Mungu basi ameweka kura yake mahali sahihi na kamba zake zimeangukia mahali pema.

Laiti kama maandiko yasemavyo watu wangeyachukulia kwa umakini mahangaiko yangekoma.

Mungu hakusikii kwa sababu umefunga na kuomba sana la! Bali anakusikia kwa sababu umeelewa Neno lake.

Ufunuo1:1 “Ufunuo wa Yesu Kristo, aliopewa na Mungu awaonyeshe watumwa wake mambo ambayo kwamba hayana budi kuwako upesi; naye akatuma kwa mkono wa Malaika akamwonyesha mtumwa wake Yohana; “

Ufunuo ni wa Yesu, mwenye Ufunuo huo ni Mungu na Yeye amempa Yesu ili awape watumwa wake. Siku ukielewa umeshinda, hauhitaji kufunga na kulia sana ili upate, hakuna hata mmoja anayestahili au asiyestahili kupokea bali tunapokea kwa sababu tumekubali kupokea.

Sio kwamba unapokea kwa sababu wewe ni bora sana au haupokei kwa sababu wewe si bora, la! Ili upokee ya Mungu haitokani na dhambi zako au kwamba hauna dhambi bali inatokana na Maamuzi yako umeamua nini leo na sio jana, inawezekana jana umetenda dhambi nyingi lakini Je! leo umeamua nini?.

Ufunuo sio mali yetu bali ni mali ya Mungu, anatuletea sisi tunaomwamini ili tupate kujua yaliyo mbele yetu, sasa ukiamini kile ambacho Yeye amesema basi umepokea.

Ufunuo 1:3 “Heri asomaye na wao wayasikiao maneno ya unabii huu, na kuyashika yaliyoandikwa humo; kwa maana wakati u karibu.”

Je! Wewe umesoma au umesikiliza? Basi una heri wewe usomaye na wewe usikiaye.

Watu wengi wanasikia na kuona lakini bado wanateseka, tatizo liko wapi? Lipo katika Mapenzi ya Mungu.

1 Yohana 5: 14 “Na huu ndio ujasiri tulio nao kwake, ya kuwa, tukiomba kitu sawasawa na mapenzi yake, atusikia.”

Ukiomba kitu sawa sawa na Mapenzi ya Mungu utapata unachoomba, tatizo lipo katika Mapenzi, Je upo kwenye Mapenzi yake? Sio kuimba, kushangilia wala kuomba bali ni Mapenzi yake.

Yohana 3:16 “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.”  Mapenzi ya Mungu kwako ni nini? Ni wewe usipotee, sasa swali linakuja, Je! Wewe unaishi maisha ya upotevu? Kama hauishi maisha ya upotevu basi omba lolote na Yeye atakupa.

1 Yohana 5:16 “Na kama tukijua kwamba ATUSIKIA, tuombacho chote, twajua kwamba tunazo zile haja tulizomwomba.” Nini maana ya Kusikia? Kusikia maana yake ni Kukubali.

Siku zote, wakati wote na muda wote Mungu ni Pendo; Kwa sababu ya Usingizi ulionao au Ujinga uliopo kichwani ndio maana unafikiri kuwa Mungu hataki kukujibu maombi yako, unapaswa kuelewa kuwa Mungu ni Pendo na Yeye anapenda watu, ukisema kuwa hataki kujibu maombi yako hiyo ni akili yako ila Yeye anakupenda.

1 Yohana 5: 14 “Na huu ndio ujasiri tulio nao kwake, ya kuwa, tukiomba kitu sawasawa na mapenzi yake, atusikia.”

Je! unakubali kuwa Mungu anakusikia? Kabla haujaomba lazima kwanza uwe na uhakika kuwa anakusikia.

  1. Kabla haujaomba tengeneza mazingira ya Yeye kukusikia kwanza ili unapoomba apate kukusikia na kukujibu.
  • Unatengenezaje mazingira ya kusikiwa na Mungu? Kwa wewe kujua Mapenzi yake juu yako, Mapenzi ya Mungu kwako ni yapi? Ni wewe usipotee, tafakari Je tabia ulizonazo ni sahihi au zinakupeleka upotevuni? Je upo kwenye dhambi? Ukiona upo hivyo tengeneza toba yako ili ikuvute karibu na Yeye ili hata utakapoomba Yeye akusikie.
  • Usijichoshe kuongea na Mungu wakati mazingira yako yanafanana na ibilisi, utaishia kusema nimeomba sana lakini Mungu hanijibu, atakujibuje wakati wewe ukitoka tu kuomba unaenda kusengenya na ndani ya moyo wako kumejaa uchungu.
  • Kabla haujaongea na Mungu chochote hakikisha ndani ya moyo wako kuna neno ambalo umelisoma na neno hilo ni kweli na akili yako na moyo wako unakubali kuwa hiyo ni kweli yako.
  1. 1 Yohana 5:16 “Na kama tukijua kwamba ATUSIKIA, tuombacho chote, twajua kwamba tunazo zile haja tulizomwomba.”
  • Jambo la pili ambalo unapaswa kuwa nalo ni wewe kukubali kuwa hapo ulipo Yeye atakusikia.
  • Kabla haujakubaliana na kuona ule ukaribu kuwa Mungu yupo karibu yako na anakusikia usiombe kitu chochote.

Lazima wewe uliyeokoka ulinde Heshima ya JINA la Mungu wako na la Bwana YESU ndipo utakapoomba lolote na Yeye atakujibu, lakini unakuta mlokole ndio wa kwanza kufanya vituko mpaka Bwana Yesu mwenyewe anashangaa, unasababisha Jina la Mungu linatukanwa na wale wasioamini hii ni mbaya.

Kwako wewe uliyeokoka onesha kwamba umeokoka kwa kulinda na kuheshimu Jina la Mungu na kufanya yaliyo Mapenzi yake kwako.

Mapenzi ya Mungu kwako ni yapi? Mapenzi ya Mungu kwako ni Wewe, sasa swali linakuja hivi, Je! wewe unafanya Mapenzi yake? Yeye amefanya Mapenzi yake Kwako na kumtoa Mwanaye wa pekee kwa ajili yako ili Wewe usipotee bali uwe na Uzima tele, Je! Wewe unafanya Mapenzi yake?.

Nehemia 1:4 “Hata ikawa niliposikia maneno hayo, nikaketi, nikalia, nikaomboleza siku kadha wa kadha; kisha nikafunga, nikaomba mbele za Mungu wa mbinguni;”

Hapa tunaona kuwa Nehemia alikuwa akitafakari yaliyomsibu, alijuta na kusikitika katika kile kilichotokea na kuapa kuwa hatarudia. Nehemia alifanya hivyo kwa siku kadha wa kadha na siyo siku moja, baada ya hayo ndipo akajipeleka mwenyewe mahali ambapo uwepo wa Mungu upo, baada ya Nehemia kuomba hayo ndipo akapokea kile alichokuwa akiomba.

Daniel 7:1 “Katika mwaka wa kwanza wa Belshaza, mfalme wa Babeli, Danielii aliona ndoto, na maono ya kichwa chake, kitandani mwake; basi akaiandika ndoto, akatoa habari ya jumla ya mambo hayo.” Baada ya maombi ya Daniel ndipo jibu lake likaja.

Daniel 9:20-21 “Basi hapo nilipokuwa nikisema, na kuomba, na kuiungama dhambi yangu, na dhambi ya watu wangu Israeli, na kuomba dua yangu mbele za BWANA, Mungu wangu, kwa ajili ya mlima mtakatifu wa Mungu wangu;”.

Tunapaswa kuchukulia mambo ya Mungu kwa uhalisia na si katika ndoto, tunapaswa kusogea karibu na Yeye ili tuweze kuuona Wema wa Mungu kwa jinsi anavyotupenda.

Unapaswa kupata Urithi wako, ndio utaupata; lakini ni lini? Ni sasa. Kuna wengine wanakufa kabla ya kufikia Urithi wao kwa sababu gani? Kwa sababu hawachukulii mambo ya Mungu kwa uhalisia.

Daniel aliona katika ndoto na kisha akaona kwa uhalisia, Je! unataka kuona mambo ya Mungu kwa uhalisia? Unapaswa kujiandaa, Daniel alijiandaaje? Daniel 1:6-8 “……. Lakini Danieli aliazimu moyoni mwake ya kuwa hatajitia unajisi kwa chakula cha mfalme, wala kwa divai aliyokunywa; basi akamwomba yule mkuu wa matowashi ampe ruhusa asijitie unajisi.” Daniel aliamua kuondokana na mambo ya unajisi, alijiandaa mwenyewe kwa kuwa Mtakatifu.

Kushika mambo ya Mungu inahitaji Utakatifu, jiandae kwa kuwa Mtakatifu ili uweze kuyashika mambo ya Mungu.

Unajiandaaje ili uweze kupokea Vitu vya Mungu? Kwa Wewe KUSAMEHE wengine na kuwa na Moyo safi.

Mathayo 5:7-8 “Heri wenye rehema; Maana hao watapata rehema. Heri wenye moyo safi; Maana hao watamwona Mungu.” Wale wanaoweza Kusamehe wengine na wao watasamehewa, Rehemu wengine ili na wewe upate kurehemiwa na sio mwingine anapopata tatizo wewe unafurahi, uwe na Moyo safi ambao hauna hila.

Kabla haujamwambia Mungu lolote angalia kwanza nafsini mwako Je wewe umesamehe?.

Swala la Kusamehe halimuhusu yule anayesamehewa bali linakuhusu Wewe unayesamehe, ukisamehe unakuwa na uhuru mbele za Mungu lakini usiposamehe kamwe hauwezi kuwa na uhuru mbele za Mungu.

Jifunze kusamehe wengine.

Je kwani ukisamehe unapungua nini? Haupungui kiungo chochote bali cha zaidi sana wewe unakuwa huru na uzito unaondoka ndani yako.

Usikate tamaa kwa sababu ya yale yaliyokuzunguka au kwa sababu ya uchovu unaokutana nao, kumtumikia Mungu sio rahisi ni kweli kuna maumivu, machungu na dharau, lakini usikate tamaa. Yakobo hakukata tamaa katika kile alichokuwa anakitaka hakuangalia ni miaka mingapi alibadilishiwa mshahara wake lakini aliendelea kumwamini Mungu. Haijalishi nini kinatokea katika Maisha yako usikate tamaa endelea kumwamini Mungu.

Wewe ndio unaweza kuibadilisha Kesho yako, adui anaweza kumtumia yeyote yule hata mkeo au mumeo ili wewe umkosee Mungu, lakini wewe usifanye hivyo, kuna mtu unakuta anamwacha mke wake au mume wake kwa sababu tu ana tabia mbaya, acha awe hivyo alivyo lakini wewe mtazame Mungu yule aliyekupa huyo mke au mume, kama ataamua kukuacha muache akuache lakini wewe usifanye hivyo.

Usimkosee Mungu kwa sababu tu rafiki yako amemkosea, inasikitisha unakuta mtu mmoja akikosea na mwingine anaiga, lakini wewe usifanye hivyo bali iangalie safari yako na Mungu wako. Hamkuzaliwa tumbo moja kila mtu alikuja kwa wakati wake huku duniani hivyo wewe mpendeze Mungu wako, mtu mmoja asikufanye ukamkosea Mungu wako.

 

 

Maoni