INJILI NA MAZINGIRA YA MTU.
INJILI NA MAZINGIRA YA MTU.
Paulo
alikuwa mwaminifu katika dini yake ya Kiyahudi aliyokuwa nayo, Bwana akamgeuza
na kumuingiza upande wa pili yaani upande wa Yesu ili aweze kufanya vizuri
upande huu; tunamuona Paulo hata alipoingia upande wa Yesu alisimama na
kuihubiri injili kwa uaminifu, kuna watu ambao wana roho au tabia ya uaminifu
ndani yao hata kabla hawajaokoka, Mungu wa Mbinguni anamgeuza huyo mtu ili
apate kumwabudu Mungu wa kweli na kutenda vizuri na kwa uaminifu wote.
Unaweza
kumkuta mtu anatamani kusonga mbele lakini kuna watu wanamzuia asisonge mbele,
unapaswa kuwa mwaminifu ili Mungu asimame na wewe na kukupa wepesi wakusonga
mbele.
Kile
ulichonacho usikubali kukaa nacho chini wala kuzimia moyo simama kwenye kile
ambacho Mungu amekupa nawe utatokeza.
Kuna
mtu ndani yake ana kitu kizuri inaweza ikawa ni uimbaji lakini akitamani kuimba
kuna mtu anakuja na kumwambia hauwezi, kama Mungu alikupa hicho simama katika
uaminifu naye Mungu atakufanya utokeze mahali kwa ajili ya utukufu wake.
Daudi aliweza kuwa mfalme wa Israel kwa
sababu ya Goliati, kwa nini? Kizingiti kikubwa cha Israel kilikuwa ni Goliati,
kwa sababu hiyo ili Mungu ajipatie mtu mwaminifu asiyeogopa ni lazima aweke
kizingiti mbele ili huyo mtu apate kukivuka na Mungu apate kujitwalia mtu huyo.
Kipawa ulichonacho hakiwezi kutokeza au kuchanua bila kuwekewa kizingiti mbele
yako, kile kizingiti kinachowekwa mbele yako siyo kwa ajili ya kukumaliza bali
ni ili uvuke upate kusonga mbele.
Kuna mahali uliwekewa kizingiti na ukashindwa
kukivuka, ni lazima ufike mahali utambue ninani aliyekupa hicho kipawa ili
uvuke kizingiti na kusonga mbele.
Kuna wakati ulipoteza wito wa Mungu ndani
yako na ukaanza kuona mambo hayaendi ukaanza kuuliza kwa nini mambo hayaendi ni
kwa sababu ulikata tamaa, leo inuka na usonge mbele, vuka vizingiti ili uweze
kufikia ukuu ambao Mungu amekukusudia.
Daudi alipojitokeza na kumpiga Goliati Taifa
zima la Israeli walishangaa yule mtu aliye watishia amekwisha kufa, baada ya
Daudi kumuua Goliati watu wote wa Israeli walijapanga katika sifa na kumsifu
Daudi, ukiona umefanya jambo fulani na watu wakaanza kukusifia hakikisha
unamrudishia Mungu utukufu wote.
Wewe unakwenda kumuua Goliati wako ambaye
anakutesa, inuka sasa jipe ujasiri vaa silaha za Mungu na usimame ili upate
kushinda.
Sauli aliposikia wana wa Israel wanamwimbia
na kumsifu Daudi akaogopa kwa kuwa alijua ufalme wake unakwenda kwa Daudi na
ndipo akataka kumuua Daudi. Unapo fanya jambo ambalo wengine wameshindwa
kulifanya hakikisha unakaa vizuri kwa maana wapo ambao watataka kukuangusha ili
usije ukafika kule ambapo Mungu amekukusudia.
Vizingiti vinavyowekwa mbele yako siyo kwa
ajili ya kukuangamiza, la! Bali vipo kwa ajili ya kukuvusha, Daudi alikutana na
vizingiti ili vimvushe kutoka katika kuchunga kondoo wa baba yake ili aweze
kusimama kwa ajili ya Taifa zima la Israeli.
Jambo lolote ambalo Mungu ameliweka katika
maisha yako na wewe ukalisimamia kwa uaminifu hakuna mtu atakayeweza kukunyang’anya.
Mahali unapopita kwenye misukosuko na hali
ngumu hauoni hata muelekeo inaweza kuwa ni ugonjwa uliokuwa nao umefika hali
hata unajiona kuwa unakufa, unapaswa kujua kuwa katikati ya hayo masumbufu
ndipo Bwana anajitokeza, weka imani yako kwake naye ataonekana kwako.
Kuna watu baada ya kuokoka wanaogopa kwenda
hata nyumbani kwao kwa sababu wanaogopa kuwa wanaweza kulogwa, sikia nikwambie
usiogope wala usiangalie mazingira yao simama kinyume nao simama katika mamlaka
uliyopewa na ujitokeze mbele yao na Mungu atakuwa pamoja na wewe, acha uoga.
Usiwe muoga kwa sababu mchawi hana nguvu kuliko Mungu uliyenaye.
Injili ya Yesu inapofanya kazi yake ikifika
katika mazingira ya mtu, inabadilisha mazoea ya huyo mtu na kumleta kule ambapo
Mungu anataka, ukiingia katika msingi ule ambao Mungu anataka ndipo sasa hiyo
injili inaanza kukurekebisha kutoka katika yale ambayo unafanya na kuona ni
faida na kumbe ni hasara.
Kama wewe nyumbani mwako hauwezi kuangalia
watoto au mke wako anaishije, basi wokovu wako ni sifuri, Lazima uwajali watu
wa nyumbani mwako kwanza. Katika mazingira yoyote unayopitia uwe mwaminifu
mbele za Bwana na mwisho wa siku kitatokeza mwisho wa safari yako.
Ombi
Mwambie
Bwana kunakipawa ulinipa ili kinipe faida lakini sikioni kwa sababu nimejawa na
kiburi kinachosababisha kipawa changu kipotee, ninakuomba Bwana Yesu
unibadilishe ili kile kipawa change kipate kuonekana.
WAKATI WA KUGEUKA NA KUDADISI
Maisha
ya wokovu tuliyonayo ni mazuri na ni matamu kama utazingatia.
Kutoka
3:1-8 “Basi huyo Musa alikuwa akilichunga kundi la Yethro
mkwewe, kuhani wa Midiani; akaliongoza kundi nyuma ya jangwa, akafika mpaka
mlima wa Mungu, hata Horebu. Malaika wa Bwana akamtokea, katika mwali wa
moto uliotoka katikati ya kijiti; akatazama, na kumbe! Kile kijiti kiliwaka
moto, nacho kijiti hakikuteketea. Musa akasema, Nitageuka sasa, niyaone
maono haya makubwa, na sababu kijiti hiki hakiteketei. Bwana alipoona ya
kuwa amegeuka ili atazame, Mungu akamwita kutoka katikati ya kile kijiti, akasema,
Musa! Musa! Akasema, Mimi hapa. Naye akasema, Usikaribie hapa; vua viatu
vyako miguuni mwako; maana mahali hapo unaposimama ni nchi takatifu. Tena
akasema, Mimi ni Mungu wa baba yako, Mungu wa Ibrahimu, Mungu wa Isaka, na
Mungu wa Yakobo. Musa akaficha uso wake; kwa maana aliogopa kumwangalia
Mungu. Bwana akasema, Hakika nimeyaona mateso ya watu wangu walioko Misri,
nami nimekisikia kilio chao kwa sababu ya wasimamizi wao; maana nayajua maumivu
yao; nami nimeshuka ili niwaokoe na mikono ya Wamisri, niwapandishe kutoka
nchi ile, hata nchi njema, kisha pana; nchi ijaayo maziwa na asali; hata mahali
pa Mkanaani, na Mhiti, na Mwamori, na Mperizi, na Mhivi, na Myebusi.”
Mungu
alikuwa anamuandaa Musa kwa ajili ya kazi, Musa aliandaliwa kwa mazingira ya
ajabu sana alitakiwa kuuwawa alipokuwa mdogo lakini alipata Neema ya kufichwa
kisha akalelewa katika nyumba ya kifalme na akapata mafunzo ya kifalme.
Musa
alikimbia akiwa na miaka 40 na akakaa jangwani kwa muda wa miaka 40 na baada ya
hapo ndipo akakutana na Mungu na kumpa majukumu ya kufanya. Usiseme kuwa
umechelewa katika utumishi wako kwa sababu unamiaka mingi, hapana kwa Mungu
hakuna kuchelewa bali kilajambo lina majira yake.
Musa
alipokuwa kule jangwani akichunga mifugo ya mkwewe ndipo akaona kijiti kikiwaka
moto; Baada ya Musa kukiona kile kijiti ndipo akasema “Nitageuka sasa,
niyaone maono haya makubwa”. Musa kwanza kabisa
alisimama, akageuka na kudadisi kile kijiti, Mungu akitaka kumtumia mtu yeyote
kwanza atamuwekea ishara fulani ambayo itamfanya avutiwe na akisha vutiwa
afanye maamuzi ya kugeuka, ili Mungu aweze kufanya naye kazi. Ili Mungu apate
kukutumia lazima uwe mdadisi wa kile ulichokiona mpaka kikakuvutia wewe uokoke.
Waliyokuwa
tayari kudadisi ndiyo waliyogundua siri za Mungu, uponyaji na maajabu ya Mungu
katika wokovu wao kwa sababu walichukua hatua ya kugeuka na kudadisi.
Watu
waliyo na kiu ya kudadisi mambo ya Mungu ndio wale ambao Mungu anaona kuwa
wameelewa na anaweza kufanya nao kazi.
Mungu
aliposema na Musa kwa ishara Musa alielewa na akaamua kugeuka na akamuona Mungu
kupitia hiyo ishara aliyoiona, sasa je! wewe Mungu hakukuonesha ishara? Mungu
alikuonesha ishara wala haukuiona lakini leo hii unataka Mungu aseme na wewe.
Mungu
alipokuonesha ishara kwa kukuponya je! Ulikaa chini na kudadisi kwa nini alikuponya?
Mungu alipoamua kuondoa dhiki zako na ukaanza kuziona Baraka zake je! Ulikaa
chini ukatafakari au ulichukulia ni kawaida tu? Mungu anakuonesha ishara kuwa
Yeye yupo, ndio maana akaondoa vita katika ndoa yako, akakuondoa kunako
umaskini, je! Mungu alipokuonesha ishara hizo wewe ulikaa chini na ukatafakari?
Ili
uweze kujua uweza wa Mungu na utendaji wake ni lazima uamue kugeuka na
kudadisi. Musa alikuwa na kiu ya kukutana na Mungu ndiyo maana akaamua kuchukua
hatua ya kugeuka.
Je
wewe haukuona ishara, au bado unaangalia umaskini unaokutesa au bado unaziendea
njia zako za kale? Musa alipoamua kugeuka alikiangalia kile kijiti na akakaza
macho yake sawasawa ili ayaone maono ya Bwana. Amua kugeuka na kukaza macho
yako sawasawa ili upate kuona kile Bwana alichokuandalia.
Wana wa Israel walipokuwa jangwani hawakuweza
kuendelea mbele kwa sababu hawakuwa na maono mazuri na ile nchi wanayoiendea
bali walikuwa na mawazo juu ya lile jangwa wanalo lipitia. Ukiamua kugeuka ili
upate kuyaona maono yako usifanye mchezo na wokovu wako, usiwe mtu wa kurudi
nyuma wala usifanye mchezo na Mungu wako, kwa maana kwa wewe kufanya hivyo
hautaweza kukipata kile ambacho Mungu amekiandaa kwa ajili yako.
Unahitaji kuamini kile ambacho umekiona na
usiondoe macho yako katika hicho ndipo Mungu atakuwa tayari kufanya kazi wewe.
Kutoka 3:4 “Bwana alipoona ya kuwa
amegeuka ili atazame, Mungu akamwita kutoka katikati ya kile kijiti, akasema,
Musa! Musa! Akasema, Mimi hapa.”
Mungu alipomuona Musa ameamua kugeuka ili atazame ndipo Mungu akamwita Musa kwa
jina lake ili ampatie maagizo, je! unataka Mungu akuite kwa jina lako? Amua
kugeuka, Je! unataka mwaka huu wa utambulisho Mungu akakutambulishe? Amua
kugeuka na kukaza macho yako katika kumtazama YEYE, acha kuangalia mazingira
unayoishi au uliyotokea kwa maana ukiyatazama hayo yatakukatisha tamaa. Yamkini
umetokea katika familia ya kimasikini, babu na baba yako ni masikini sasa
ukiwatazama hao kamwe hautaweza kufika kule ambapo Mungu amekukusudia, kaza macho
yako kwa Bwana YEYE aliye muweza wa yote ili uweze kuyapata yale aliyoyaandaa
kwa ajili yako.
Mungu
hakumtafuta Musa akiwa kati kati ya watu bali alimtafuta akiwa pekeyake, kama
unataka kumuona Bwana kaa peke yako.
Maoni